Mkulima library ni kitengo kinachotoa huduma ya habari na taarifa kwa wakulima hapa nchini Tanzania na hata nje ya nchi, ambacho kimeanzishwa na Maktaba ya Taifa ya Kilimo ya Sokoine iliyo chini ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA).

Umuhimu wa kilimo nchini Tanzania ni mkubwa kwa kuwa unabeba uti wa mgongo wa uchumi wa nchi hii tangu enzi za zamani hata leo, na kwa ajili hii kitengo hiki cha aina yake kinawaangalia wakulima kama sehemu muhimu katika uchumi wa taifa. Kwa hiyo kitengo kimejikita katika kutoa kwa mapana huduma ya habari na taarifa za kilimo kwa wakulima mmoja mmoja na sekta binafsi kwa kutumia mtandao wa teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA). Nia ni kutoa taarifa kulingana na mahitaji ya wakulima nchini kote ikiwa ni pamoja na maeneo ya vijijini ambako huduma nyingi za taarifa na habari hazifiki wa urahisi. Huduma hii itawezesha wakulima kupata taarifa muhimu za ugani na nyinginezo kufuata matakwa ya wahitaji wa taarifa hizo ili zitumike katika kuinua kilimo na uchumi wa mtu binafsi hata wa taifa zima kwa ujumla. Wakulima wanaweza kupata taarifa hizi kwa ama kutembelea tovuti ya kitengo...., au kwa kufika moja kwa moja katika Maktaba ya SUA ambapo watakutana na huduma ya kiuweledi itakayokidhi mahitaji yao ya taarifa husika.

Pamoja na watumiaji/wahitaji wa taarifa kujihudumia wenyewe kwa njia ya mtandao, pia kitengo kinatoa mafunzo ya mtu mmoja mmoja au vikundi kwa muda mfupi ya namna ya kutumia njia za kisasa za TEHAMA kupata taarifa na habari mbalimbali, kutoa rufaa au huduma ya maelekezo ya mahali pa kupata msaada wa zaidi kufuatana na uhitaji wa taarifa ulivyo.

Maktaba ya Taifa ya Kilimo ya Sokoine inapenda kuchukua fursa hii kutangaza kuanzishwa kwa “Mkulima Library” pamoja na kuwakaribisha wote kuitumia katika kujipatia habari, taarifa na maarifa ya Kilimo chenye tija.

Copyright © 2020 Sokoine National Agricultural Library. All Rights Reserved